HALI YA KISIASA MKOANI KIGOMA.
https://alloycenyanda.blogspot.com/2015/10/hali-ya-kisiasa-mkoani-kigoma.html
MWANDISHI: JUMA SHABANI
MAHALI: KIGOMA.
Hii ni makala maalumu ya
kiasiasa kuelekea uchaguzi mkuu ambao utachambua kwa kina hali ya kisiasa
mkoani hapa kwa kila Nyanja huku tukipitia matukio ya nyuma kama kioo cha kuangalia
nini kitatokea katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Makala hii itaangazia kwa
ujumla hali ilivyo sasa kisiasa na ilivyokuwa na kuakisi matarajio ya wananchi
wa Kigoma katika uchaguzi huu. Makala hii itachunguza kwa kina ubora wa sera,
wagombea na uelewa wa wananchi katika kufikia jukumu kubwa la kuchagua hapo
Oktoba 25, 2015.
MKOA WA KIGOMA KWA UJUMLA.
Mkoa wa Kigoma una ukubwa wa
eneo la kilometa za mraba 45,066 sawa na asilimia 4.8 ya eneo lpte katika
jamuhuri ya muungano wa Tanzania. Kulingana na sense ya mwaka 2012, mkoa wa
Kigoma una wananchi wanaofikia 2,127,930.
Mkoa wa Kigoma una wilaya za
Kigoma, Uvinza, Kasulu, Buhigwe, Kibondo na Kakonko. Mkoa huu una majimbo ya
Kigoma Mjini, Buhigwe {Manyovu}, Kasulu Vijijini, Kasulu Mjini, Buyungu, Muhambwe,
Kigoma Kaskazini na Kigoma Kusini. Mkoa wa Kigoma una kata 139 zenye wapiga
kura 774,941.
Kwa mujibu wa tume ya
uchaguzi, Mkoa wa Kigoma uliandikisha wapiga kura 774,941 sawa na 83% ya
makadirio ya tume ambayo ni sawa na 75.1% ya makisio ya NBS.
MKOA WA KIGOMA NA HISTORIA YA
UCHAGUZI WA VYAMA VINGI.
Mkoa wa Kigoma ni mkoa wa
mwanzo kabisa kufanya siasa za vyama vingi mapema mwaka 1994 baada ya uchaguzi
mdogo ulifanywa mwaka huo baada ya aliyekuwa mbunge wa jimbo la Kigoma Mjini Ibrahim Mbano kufariki dunia.
Huu ndio uchaguzi wa kwanza
wa vyama vingi kufanyika ambapo kwa mara ya kwanza ilikuwa jaribio la aina mpya
siasa mjini. Katika uchaguzi huu mambo kadhaa yalijitokeza ambapo Dr. Aman
walid Kabourou aliingia kwa mara ya kwanza kwenye siasa akitokea nchini
marekeni. Uchaguzi huo pamoja na kushirikisha vyama vingi ila ni vyama vya CCM
na Chadema vilivyokuwa na ushindani wa hali ya juu ambapo kwa CCM alisimamishwa
Ndugu Azim dewji na kwa Chadema alisimamishwa Kabourou.
Matokeo ya uchaguzi huo
yalionesha ishara njema kwa siasa za vyama vingi ambapo CCM ilishinda kwa kura
chache sana na Chadema kupitia Kabourou walikwenda mahakamani kupinga ambapo
uchaguzi ulitenguliwa kabla ya Azim kukata rufaa. Kwakuwa mwaka 1995 ulikuwa
unakaribia na uchaguzi mkuu kuitishwa, hivyo jimbo lilikaa bila mbunge kwa
mwaka wa 1994 maana kesi ilikuwa mahakama ya rufaa.
Mwaka 1995 ilikuwa mwaka wa
kwanza wa uchaguzi mkuu wa vyama vingi ambapo kwa Kigoma tayari kulikuwa na
uzoefu wa siasa za vyama vingi. Wakatai wengine wanaanza kuona faida na hasara
ya siasa za vyama vingi, kwa Kigoma hakukuwa na jipya sana. Watu kwa makundi
walikuwa na kesi za uchagu, wengine walishapigwa na polisi na mambo kadhaa ya
kisiasa za ushindani yakiwa yameshaonekana.
Pamoja na kuwa kulikuwa na
vyama vingi sana vilivyosimamisha wagombea mkoani hapa zaidi ya mikoa mingi
nchi hali iliyoashiria kupokelewa kwa vyama vingi mkoani ila vyama viwili vya
CCM na Chadema ndio vilikuwa na nguvu mkoani hapa. Ni kipindi hiki ambapo
wanakigoma walipokea mabadiliko chini ya NCCR na Mrema katika ngazi ya Urais
ila walibaki na misimamo katika vyama vyao vya CCM na Chadema. Kwa ngazi ya
ubunge, mara ya kwanza Mkoani hapa jimbo la Kigoma Mjini lilipata mbunge wa
upinzani huku kata nyingi pia zikienda upinzani.
Hali ya kisiasa mkoani Kigoma
imekuwa haitabiliki ambapo katika majimbo mengi upinzani na CCM wamekuwa
wakipokezana kuongoza. Mfano wa majimbo hayo ni Kigoma Mjini, Kigoma Kusini,
Kigoma Kaskazini na mwaka 2010 majimbo ya Kaulu na Kibondo Mjini yalichagua
upinzani kwa mara ya kwanza.
CCM imebaki kuwa chama chenye
nguvu mkoani humu ambapo kura za urais kwa miaka yote zimekuwa zikiongozwa na
CCM, huku wabunge wengi wa jimbo hili wakitokea CCM. Pia, mkoa huu umebahatika
kutoa mawaziri na manaibu mawaziri katika serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
MUAMKO WA WANANCHI
Uchaguzi wa mwaka huu umekuwa
na muamko wa hali ya juu ambapo mkoani hapa kumekuwepo na vyama vinne vyenye
nguvu ya kiushindani. Vyama hivyo ni CCM, Chadema, ACT na NCCR Mageuzi. Hivyo
kwa mara ya kwanza kama alivyosema Mh, Mbowe mwenyekiti wa Chadema na
Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa alipoiona hali ya kisiasa mkoani Kigoma alisema
“Natambua mwaka huu hapa kuna ngoma nzito”
Makala hii inasitishwa hapa
kwa leo. Mwisho wa makala hii kwa leo ni mwanzo wa makala nyingine kesho ambapo
nitaanza kuchambua kwa kina hali ya kisiasa ilivyo kuelekea uchaguzi mkuu 2015
katika ngazi ya Urais.
